UN: Waliowafanyia unyama mahabusu wa Kipalestina katika jela za Israel wawajibishwe
UN: Waliowafanyia unyama mahabusu wa Kipalestina katika jela za Israel wawajibishwe
Aug 08, 2024 07:33 UTC
Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi wa Kipalestina (UNRWA) amesema lazima kuwepo na uwajibishaji dhidi ya ukiukaji wa haki Wapalestina wanaoshikiliwa katika magereza ya utawala wa Kizayuni wa Israel.
Philippe Lazzarini ameeleza hayo katika ujumbe alioweka
kwenye mtandao wa X na kusisitiza kwa kusema: "ubinadamu uko katika hali
mbaya zaidi".
Lazzarini amesema UNRWA imeguswa na "mienendo isiyo ya kibinadamu"
waliyofanyiwa mahabusu Wapalestina mnamo mwezi Aprili katika vituo vya
mahabusu vya Israel.
Akiashiria ripoti ya hivi karibuni ya ofisi ya haki za binadamu ya
Umoja wa Mataifa kuhusu vitendo hivyo pamoja na ripoti ya Kituo cha
Habari cha Israel cha Haki za Binadamu katika maeneo yanayokaliwa kwa
mabavu (B'tselem), Lazzarini amesema ripoti hiyo imezungumzia sera ya
kimfumo na ya makusudi ya kudhalilisha utu na mateso dhidi ya
Wapalestina na akaongeza kuwa ni vigumu sana mtu kuweza kuisoma ripoti
hiyo.
Mkuu huyo wa UNRWA amebainisha kuwa: "hakuna anayeachwa, hakuna aliye salama hata huko Israel," na akasisitiza kwa kusema: "waliohusika lazima wawajibishwe. Manusura lazima watendewe haki."
Vyombo kadhaa vya habari vya Israel vilisambaza mkanda wa video
unaohusisha wanajeshi wa Israel wanaodaiwa kumbaka mfungwa wa
Kipalestina katika Gereza la Sde Teiman katika jangwa la Negev kusini
mwa Israel.
Mwishoni mwa mwezi uliopita, wanajeshi 10 walikamatwa kwa madai ya kumbaka Mpalestina anayeshikiliwa katika kituo hicho.
Ripoti kadhaa zimeibuka kuhusu unyanyasaji mkali
wanaofanyiwa wafungwa wa Kipalestina tangu yalipoanza mashambulizi ya
kinyama na mauaji ya kimbari ya utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya
Ukanda wa Ghaza.../
Comments
Post a Comment